Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel amefanya kikao kazi na watumishi wa Idara ya Kinga kikiwa na lengo la kupeana taarifa za kiutendaji na kujadili muelekeo wa huduma za kinga dhidi ya magonjwa mbalimbali ikiwemo magonjwa ya Kifua Kikuu na Ukoma. Kikao hicho kilichofanyika katika Hospitali ya Benjamini Mkapa, Jijini Dodoma.
Katika kikao hicho Mhe. Naibu Waziri aliwaasa watumishi wa Idara ya Kinga kujikita katika kutekeleza majukumu yao kwa uweledi, uadilifu na kwa kuzingatia mikakati yenye kulenga kutatua matatizo ya wananchi ikiwemo upatikanaji wa dawa na vifaa tiba na utoaji wa huduma bora za afya. Aidha, amewaasa pia watumishi wa Idara ya Kinga kulinda taswira ya Wizara ya Afya wanapotekeleza majukumu yao katika ngazi zote.
Katika hatua nyingine, Mkurugenzi wa Huduma za Kinga Dkt. Beatrice Mutayoba alisema Idara yake imepiga hatua kwenye kupunguza idadi ya vifo vitokanavyo na magonjwa ya kuambukiza ikiwemo Kifua Kikuu na UKIMWI. Pia, alimshukuru Mhe. Naibu kwa kupata wasaa wa kuzugumza na watumishi na kuahidi yale yote aliyoyaelekeza watayafanyia kazi ili kuleta tija na ufanisi katika kutoa huduma bora za afya hususani Kinga.
Idara ya Kinga inajumuisha sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma, Huduma za Lishe, Epidemiolojia na Udhibiti wa Magonjwa, Afya Mazingira na Usafi pamoja na Programu za UKIMWI, Malaria, Kifua Kikuu na Ukoma, Chanjo na Magonjwa Yasiyopewa Kipaumbele.